KAMBI YA WAPIGANIA UHURU YA FARM 17 NACHINGWE | LI...
KAMBI YA WAPIGANIA UHURU YA FARM 17 NACHINGWE | LINDI
Tanzania
KAMBI YA 17 – KAMBI YA WAPIGANIA UHURU
Kambi ya Farm 17 iliyopo takribani kilomita 34 kutoka Mji wa Nachingwea, Mkoa wa Lindi, ni moja ya maeneo muhimu ya urithi wa ukombozi wa Bara la Afrika nchini Tanzania. Eneo hili lilitumika kama kambi kuu ya mafunzo ya kijeshi, makazi na uratibu wa harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika katika miaka ya 1960 na 1970. Kwa sasa, Shamba 17 ni sehemu ya maeneo ya urithi yanayosimamiwa na Kituo cha Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika (ALHC).
Awali, Kambi ya Farm 17 lilianzishwa katika kipindi cha Mradi wa Karanga wa Waingereza (British Groundnut Scheme) mwishoni mwa miaka ya 1940. Baada ya Tanzania kupata uhuru mwaka 1961, Serikali ya Tanzania ililibadili eneo hilo na kulifanya kuwa kituo muhimu cha mafunzo kwa wapigania uhuru kutoka nchi mbalimbali za Kusini mwa Afrika waliokuwa wakipambana dhidi ya ukoloni na ubaguzi wa rangi.
Kambi ya Farm 17 ilitumika na harakati mbalimbali za ukombozi, zikiwemo:
FRELIMO (Msumbiji)
MPLA (Angola)
ZANLA – ZANU (Zimbabwe)
ZIPRA – ZAPU (Zimbabwe)
ANC (Afrika Kusini)
Maelfu ya wapigania uhuru walipata mafunzo ya kijeshi na kisiasa katika kambi hii kabla ya kurejea kupigania uhuru wa mataifa yao.
Miongoni mwa maeneo ya kihistoria yaliyopo Kambi ya Farm 17 ni:
Nyumba ya kihistoria aliyotumia Samora Machel.
Handaki la ulinzi lenye urefu wa takribani kilomita tatu lililotumika wakati wa mafunzo na shughuli za kijeshi.
Viwanja vya mafunzo ya wapigania uhuru.
Majengo ya kihistoria yaliyojengwa wakati wa Mradi wa Karanga wa Waingereza.
Shule ya Sekondari ya Kambi Farm 17, inayopatikana ndani ya eneo hilo huku ikihifadhi sehemu ya historia ya ukombozi.
Kambi ya Farm 17 ni alama ya mshikamano wa Afrika na ushahidi wa mchango mkubwa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuunga mkono harakati za ukombozi wa Bara la Afrika. Eneo hili linaendelea kuhifadhiwa kama urithi muhimu wa kihistoria kwa ajili ya elimu, utafiti na utalii wa urithi kwa vizazi vya sasa na vijavyo.